*FAIDA ZA KAZI* inaendelea.....
4. KAZI ITAIMARISHA AFYA YAKO
Katika sehemu nyingi mbalimbali duniani imeanza kuonekana kwamba akina mama huwa na maisha marefu zaidi kuliko akina baba. Kuna sababu mbalimbali ambazo huleta tofauti hiyo, na mojawapo ambayo wataalam wengi wanakubaliana nayo ni ile inayohusu kazi. Wanasema kwamba kwa vile kina mama wanafanya kazi zaidi kuliko kina baba (yaani hawastaafu kufanya kazi ya kupika au ya kutunza usafi wa nyumba) miili yao inapata nafasi kubwa ya kufanya mazoezi na kuimarika. Ni dhahiri kwamba kazi mbalimbali hutoa nafasi ya kutosha kwa mazoezi ya viungo mbalimbali vya mwili. Ukikaa bila kazi za kutosha mwili huchakaa upesi zaidi. Hata hivyo yafaa ukumbuke kwamba kazi ni lazima ziwe za kiasi. Zikizidi mno au zikiwa nzito mno mwili utashindwa kuzimudu, na matokeo yake yatakuwa ni afya mbaya na maisha mafupi. Vile vile usisahau kwamba kuna chache fulani fulani ambazo huweza kudhuru afya endapo tahadhari maalum hazitachukuliwa wakati wa kuzifanya k.m. uchimbaji wa baadhi ya madini fulani fulani, au ufanyaji kazi katika mazingira yasiyofaa, n.k.
*** Mwisho wa Faida za Kazi ***
KWA NINI NI LAZIMA TUFANYE KAZI
Katika maelezo yaliyotangulia tumeona faida unazoweza kupata kutokana na kufanya kazi. Pamoja na faida hizi kuna sababu nyingine
*'muhimu'* ambazo zinakulazimisha ufanye kazi ukipenda usipende. *Wazazi wako na jamaa wengine wanakutazamia ufanye kazi ili uwape nafasi ya kupumua.* Hawawezi kuendelea kukutumikia wakati wote. Kuna kikomo cha utumishi wao kwako. *"Hata kama huoni aibu kuendelea kusaidiwa saidiwa nao, yafaa ukumbuke kwamba utafika wakati ambao uwezo wao utapungua, nawe mwenyewe itabidi uchukue jukumu la kuwasaidia.*
Zaidi sana wazazi na jamaa zako wanakutazamia ufanye kazi ile uweze kujipatia maendeleo yako mwenyewe katika jamii. Kwa mfano wanakutazamia uoe au uolewe, na ujipatie nyumba na watoto wako mwenyewe. Hayo yatatoka wapi bila kazi? *Si haki, wala si vizuri wazazi na jamaa zako wakushughulikie katika mambo kama hayo.* Unapaswa ujilishe wewe mwenyewe na watoto wako kwa jasho lako bila kutegemea msaada toka kwa wengine.
Jamii na taifa, nao kwa upande wao wanakutazamia ufanye kazi ili usiwe mzigo kwao. Watu wanaozurura ovyo bila kazi mara nyingi huonekana wanapendelea kuwa wahalifu wa sheria, au walalamikaji, au wenye kutaka kuleta *mapinduzi* yasiyo na msingi wa maana katika maendeleo ya nchi.
Hivyo licha ya kupunguza mzigo na wasiwasi kwa jamii na taifa lako, wewe mwenyewe unaweza kusaidia pia kuongeza uchumi wa nchi yako kama utaamua kufanya kazi badala ya kuzurura ovyo. Taifa na jamii wanakutazamia ukuze uchumi na maendeleo ya nchi, sio tu kwa faida ya wengine, bali kwa faida yako mwenyewe. Je, ukiugua utatibiwa? Unadhani hizo dawa zitatoka wapi? Je, ukisafiri hutatumia vyombo vya usafiri? Unadhani vyombo hivyo vinaingia bure nchini? Huna budi ufanye kazi ikiwa unataka utoe mchango wako kwa huduma mbalimbali unazozipata katika jamii na taifa.
*Pengine mojawapo ya sababu muhimu sana ambayo inakulazimisha ufanye kazi ni ile ya kutumia kipawa chako kwa faida ya wengine.* Kwa mfano katika jamii na taifa mara kwa mara hutokea upungufu wa waalimu, madaktari, viongozi wa vijiji, viongozi wa dini, n.k. je, kama wewe una kipawa au uwezo wa kumudu kazi kama hizo, huoni ni lazima uitikie mwito wa kutumikia jamii na taifa lako ikiwa utaombwa kufanya hivyo? Kama utakataa, na wengine nao watakataa, taifa litakuwa wapi? Jambo hili tutalifikiria zaidi katika maelezo mengine hapo baadaye.