Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayotupeleka nchini Sudan Kusini kufuatilia mradi wa kilimo cha mpunga ulivyoleta ustawi kwa jamii ya katikati mwa Sudan unaofanikishwa kwa msaada wa mafunzo wa walinda amani wa UN kutoka Korea Kusini wanaohudumu katika UNMISS kupitia wanasayansi na wakulima wa eneo la Bor katika. Pia tunakuletea muhtasari wa habari na ufafanuzi wa methali.Mapigano makali mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo yamesababisha vifo vya zaidi ya raia 70, kuwafurusha watu zaidi ya 200,000, na kusitisha msaada wa chakula kwa maelfu. Umoja wa Mataifa unasema hali katika Kivu Kusini imezorota kwa kasi, huku msaada wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula WFP ukisimama na shule zaidi ya 30 zikigeuzwa makazi ya dharura. Katika taarifa yake, Naibu Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Farhan Haq, amesema hali imefikia kiwango cha hatari, akionya: “Familia zinazoishi kwa njaa sasa zinagawana chakula chao cha mwisho na watu waliokimbia makazi. Hii ni dharura inayovuka mipaka.” UN inazitaka pande zote kusitisha mapigano mara moja na kuruhusu misaada kufika kwa walio hatarini.Mkutano wa kikao cha 7 wa Baraza La Mazingira la Umoja wa Mataifa UNE-7 unaeelekea ukingoni jijini Nairobi Kenya na miongoni mwa washiriki ni kijana mwanaharakati wa mazingira kutoka asasi ya Umoja wa Mataifa YUNA nchini Tanzania Ally MwamzoraNa leo Umoja wa Mataifa unaadhimisha Siku ya Kimataifa ya Milima, ukisisitiza umuhimu wa milima kama “kitovu cha maji ya dunia.” Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO, takriban asilimia 70 ya maji safi ya Dunia yamehifadhiwa kama theluji au barafu, yakitoa mito inayosambaza maji ya kunywa, kilimo, viwanda, na umeme wa maji na takriban watu bilioni mbili, ikiwa ni pamoja na jamii nyingi za asili, wanategemea maji ya milima kwa mahitaji yao ya kila siku, maisha, na tamaduni zao. Wataalamu wanasisitiza kuwa kulinda mazingira ya milima ni muhimu ili kuhakikisha upatikanaji wa maji kwa vizazi vijavyo.Katika kujifunza lugha Kiswahili, leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi nchini Kenya, kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali "“MWENDAWAZIMU HAPEWI UPANGA"Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!