Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni, WHO, limeongoza uhamishwaji wa wagonjwa kutoka Gaza eneo la Palestina linalokaliwa kimabavu na Israeli, ikiwa ni mara ya kwanza tangu kuanza kwa awamu mpya ya kusitishwa kwa mapigano kwenye ukanda huo.Katika muda wa siku mbili, wagonjwa 41 waliokuwa katika hali mbaya pamoja na familia zao 145 wamehamishwa kutoka eneo la mgogoro, kuelekea Afrika Kusini, Uswisi na kwingineko, huku maelfu zaidi wakiendelea kusubiri matibabu ya dharura.Katika hospital iliyojengwa kwa mahema katika eneo la AL-MAWASI, RAFAH kwenye Ukanda wa Gaza wagonjwa wakihudumiwa kila kona watoto kwa wakubwa Miongoni mwao ni Ibrahim Abu Ashiba, mkurugenzi wa filamu ambaye maisha yake yamebadilika ghafla. Anakumbuka wakati alipojeruhiwa. Anasema, "Nilipigwa risasi mara kadhaa, mara moja kwenye kifua, mara moja kwenye bega, mara mbili mkononi. Risasi hizo mbili zilikata mishipa ya neva ya mkono wangu. Sasa siwezi kushika kamera wala kunyoosha mkono wangu kawaida. Ghafla, maisha yangu yote yalisimama."Safari ya kupona kwa Ibrahim inaanzia Afrika Kusini, ambapo amekubaliwa kwenda kupokea matibabu maalum ambapo anasema "Maisha yangu yote yalikuwa yamesimama baada ya kujeruhiwa hadi waliponipigia simu na kunijulishakwamba nitasafiri kwenda Afrika Kusini kwa matibabu. Ilionekana kama nimezaliwa upya."Mgonjwa mwingine katika hospitali hii ni, Maria Al-Shaer, alijeruhiwa vibaya katika mashambulizi yaliyokuwa yakiendelea Gaza, huku akipoteza ndugu zake. Mama yake, Raghda Ahmed Al Shaer, anaelezea mateso hayo. "Maria amepoteza baba yake na ndugu zake wote. Alijeruhiwa na kuvunjika mguu, mifupa na kupoteza nyama. Anahitaji upasuaji wa kuwekewa viungo bandia. Maisha yake yamegeuka, hawezi kutembea, na hali yake ya kisaikolojia imeathirika sana."Uhamishwaji huu umeratibiwa na Shirikisho la Chama cha Msalaba Mwekundu Palestina, kwa msaada wa WHO. Dkt. Luca Pigozzi, Mratibu wa Timu ya Dharura ya WHO, anafafanua umuhimu wake."Huu ni uhamishaji wa kwanza wa matibabu tangu kusitishwa kwa mapigano Oktoba 10. Tumejizatiti kuongeza uwezo wetu kusaidia na kuratibu uhamishaji kwa ajili ya matibabu, kwa ushirikiano wa karibu na Shirikisho la chama cha Msalaba Mwekundu la Palestina."Raghda anaeleza matumaini kwa ajili ya binti yake wanapohama kwenda Uswisi. "Wametupigia kutuarifu kwamba Maria amekubaliwa kusafiri kwenda Uswisi kwa matibabu. Tumefurahi sana kwamba atatembea tena, na hali yake ya kisaikolojia itaboreka. Atarudi kuwa Maria wa kawaida kama tuliyemjua."WHO inasisitiza kuwa wagonjwa takriban 15,000 bado wanangojea idhini ya kupata matibabu nje ya Gaza na inatoa wito kwa nchi zote kufungua milango yote za dharura kwa ajili ya uokoaji wa wagonjwa.