Huko Bunia, jimboni Ituri Mashariki Mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, Mkuu wa Operesheni za Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa, Jean-Pierre Lacroix, amepongeza juhudi za pamoja za walinda amani wa Mpango wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo MONUSCO na jeshi la serikali ya Congo, FARDC, katika juhudi za kulinda raia na kupunguza ghasia za makundi yenye silaha.Akizungumza wakati wa ziara yake iliyoanza Septemba 6, Mashariki mwa DRC katika jimbo la Ituri Lacroix amesema ushirikiano na kuaminiana kati ya mamlaka za jimbo la Ituri na vikosi vya Umoja wa Mataifa ni msingi muhimu wa kurejesha amani.Anasema “Nipo katika eneo liitwalo Fataki, katika jimbo la Ituri, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, na hapa kuna kambi ya MONUSCO yenye kikosi cha Nepal, pamoja na kambi ya wakimbizi wa ndani. Maelfu ya watu wanalindwa hapa na wenzetu wa MONUSCO, na wanapatiwa msaada wa kibinadamu pamoja na ulinzi.”Gavana wa Ituri, Jenerali Johnny Luboya, alikaribisha msaada wa MONUSCO katika operesheni za kijeshi na mazungumzo ya amani, yakiwemo dhidi ya kundi la CRP katika eneo la Djugu Ituri ambako mamia ya maelfu ya wakimbizi wa ndani sasa wananufaika na ulinzi wa pamoja wa FARDC na walinda amani wa Umoja wa Mataifa. Lacroix amesema “Katika jimbo la Ituri pekee kuna makambi kadhaa ya wakimbizi wa ndani, ambayo yanalindwa na MONUSCO, ambapo makumi ya maelfu kwa hakika mamia ya maelfu ya watu wanalindwa na wenzetu wa MONUSCO na wanapatiwa msaada.”Mkuu huyo wa operesheni za ulinzi wa amani ameohitimisha kwa kusema ziara hii ni muhimu sana kwani “Nipo hapa kuonyesha kile ambacho MONUSCO hufanya kila siku, tofauti ambayo MONUSCO inaleta katika kuwalinda raia hawa, tofauti kati ya kuwa salama au kuwa katika hatari kubwa, na nilitaka pia kutoa shukrani zangu kwa wenzetu wa MONUSCO. Aidha, nilitaka kuwasikiliza wananchi, hawa wakimbizi wa ndani, pamoja na jamii, na kuona namna ambavyo tunaweza kushirikiana nao zaidi ili kuboresha hali na kupiga hatua katika kukabiliana na ghasia ambazo bado zinaendelea katika eneo hilo.”Baada ya zira yake jimboni Itari Lacrix ameelekea katika mji Mkuu Kinshasa ambako amekutana na na kuzungumza na maafisa wa serikali.