Jaridani leo jaridani tunakuletea mada kwa kina kuhusu masuala ya wanawake, tathmini ya miaka 30 ya harakati za kusongesha haki za wanawake na utamsikia maoni ya Balozi Gertrude Mongella kutoka Tanzania. Pia tunakuletea muhtasari wa habari na uchambuzi wa methali.Mjadala Mkuu wa mkutano wa 80 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ukianza Jumatatu ijayo, Rais wa Mkutano huo Annalena Baerbock amewaambia waandishi wa habari jijini New York, Marekani kuwa “jukumu letu ni Umoja wa Mataifa uwe thabiti kwa miaka 80 ijayo. Michakato ya kuhakikisha hilo ndio itakuwa jukumu letu mwaka huu, ikiwemo kusongesha ajenda ya marekebisho ya Umoja wa Mataifa. Kwa hiyo tukitaka Umoja wa Mataifa thabiti, basi tunahitaji ahadi kutoka serikali zote duniani.Ripoti ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa inayotolewa kila mwaka kabla ya kuanza kwa Mjadala Mkuu wa Baraza Kuu inasema Umoja wa Mataifa umeendelea kusimama imara, ukifanya kazi ya kuendeleza amani, kuchochea maendeleo endelevu, na kupunguza mateso ya kibinadamu licha ya majaribu makubwa. Katika ripoti hiyo Antonio Guterres amesisitiza uimara wa watumishi wa Umoja wa Mataifa, ambao wamejitolea kuleta matumaini na msaada kwa wale wanaohitaji licha ya kufanya kazi katika mazingira magumu.ripoti ya Hali ya Rasilimali za Maji Duniani iliyotolewa leo inasema ni takriban theluthi moja tu ya mabonde ya mito duniani yaliyokuwa na hali ya “kawaida” mwaka 2024 ilhali mengine yote yalikuwa na kiwango cha juu zaidi cha maji au chini ya kiwango cha kawaida — ikiwa ni mwaka wa sita mfululizo wa kutokuwepo kwa uwiano wa wazi. Ikitolewa na shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa, WMO, ripoti inasema mwaka 2024 uliokuwa mwaka wa joto zaidi kuwahi kurekodiwa ulianza na tukio la El Niño ambalo liliathiri vibaya mabonde makubwa ya mito na kusababisha ukame katika maeneo kadhaa ikiwemo kusini mwa Afrika.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili, leo mchambuzi wetu ni Dkt. Josephat Gitonga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi nchini Kenya, kwenye kitivo cha Tafsiri na Ukalimani anafafanua maana ya methali "MZOEA PUNDA HAPENDI FARASI"Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!